Wednesday, April 23, 2008

Rais mtaafu Mkapa, mkewe waumbuliwa bungeni kwa mgodi wa Kiwira










MBUNGE wa Vunjo, Aloyce Kimaro (CCM), amewatuhumu Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa, mkewe Mama Anna Mkapa na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Daniel Yona, kuwa walinunua mgodi wa Makaa ya Mawe wa Kiwira, wilayani Rungwe, Mbeya kwa kificho.

Mbunge huyo alidai bungeni jana kuwa mwaka 2004, Mkapa kwa kushirikiana na mkewe pamoja na Yona, walianzisha Kampuni ya TanPower Resources Ltd na mwaka mmoja baadaye wakauziwa machimbo ya Kiwira kimya kimya.

Kimaro alitoa madai hayo alipokuwa akichangia Muswada wa Sheria ya Umeme wa Mwaka 2008, bungeni, mjini hapa juzi jioni.

Alidai kuwa katika mauziano hayo ya siri, Kampuni ya TanPower Resources Limited,
ilikuwa iilipe serikali Sh700milioni katika mradi huo uliogharimu, zaidi ya Sh4bilioni, lakini kampuni hiyo ilifanya malipo ya awali ya Sh70milioni tu.

"Waliuziwa kwa Sh700milioni bila kutangazwa na wao wakalipa down payment (malipo
ya awali)Sh70 milioni," alisema Kimaro.

Aliendelea kudai kuwa mwaka 2006, Mkapa, Anna na Yona, waliingia mkataba na Shirika la
Umeme nchini (Tanesco) kwa ajili ya kufua umeme kwa makubaliano ya kulipwa Gharama za uwekezaji ('capacity charge') Sh146milioni kila siku, bila kujali kwamba wamefua umeme au la.
"Sasa mimi nauliza huu ni uadilifu kweli? Haya ni maadili kweli? Tufike mahala
tuseme inatosha. Hivi tunawafundisha nini vijana hawa ambao ni mawaziri?," alihoji
Kimaro na kuongeza:

"Rais Jakaya Kikwete alisema urais wake hauna ubia na mtu. Basi aseme huu ni mwisho kwa wanaotuhujumu, tuwaambie basi na washughulikiwe kwa mujibu wa sheria."

Awali, akichangia muswada huo, Kimaro alisema ipo haja ya kuwa makini katika kuupitisha muswada huo kwa kuwa wawekezaji watakaokuja kuwekeza katika umeme, si rahisi kwenda vijijini kusambaza nishati hiyo.

Kutokana na hali hiyo, aliitaka serikali kuifufua Tanesco kwa kuipa fedha ili (serikali) iwe na chombo chake cha kuzalisha umeme.

Naye Mbunge wa Mpanda Kati (Chadema), Said Amour Arfi, alishangazwa namna serikali
inavyotumia nguvu nyingi kuupitisha muswada huo.

Alisema haafiki kupitishwa kwa muswada huo na kuongeza kuwa nguvu inayotumika kuharakisha kupitishwa muswada huo si ya kawaida.

Alisema hoja ya kuwa muswada huo ukipita, wananchi wa vijijini watapata umeme wa bei rahisi, haina nguvu.

Alitoa mfano wa Kampuni ya Artumas ambayo baadhi ya wabunge waliipigia debe, kwamba haitaweza kuondoa matatizo ya umeme.

Tanesco itaingiaje katika ushindani wakati ikiwa hoi? Tanesco inavishwa majukumu
ya kisiasa,? alisema na kuonya kwamba wawekezaji watakaokuja si ajabu wakafanana na hadithi ya ubinafsishwaji wa Benki ya NMB.

Alikumbusha kuwa wakati NMB inabinafsishwa, ilisemwa kuwa itakuwa benki ya wananchi
na itawafikia watu wengi, lakini leo hii ukitaka kufungua tawi vijijini wana vigezo vyao na si jambo rahisi kufika huko.

?Na hao (wawekezaji) wakija, wataweka vigezo vyao vya kusambaza umeme vijijini ambavyo havitawawezesha wananchi wa huko kunufaika na huduma hiyo,? alibainisha.

Naye Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela alimwangaliza Waziri wa Nishati
na Madini, William Ngeleja, kutambua aina ya wawekezaji wanaotarajiwa kuwekeza katika sekta ya umeme baada ya sheria mpya ya sekta hiyo kupitishwa, kwani ndiyo watakaomwangusha ama kumwinua.

?Nakupa angalizo Mheshimiwa Waziri, ujue kuwa aina ya wawekezaji watakaoingia katika sekta ya nishati ndiyo watakaokuangusha au kukuinua, wapo Watanzania wenzetu wanajiandaa kuingia katika biashara hiyo, wengine ni wale walionufaika na mikataba mibovu kama ule wa Richmond,? alitahadharisha Mbunge huyo.

Alidai kuwa baadhi ya Watanzania, hususani walionufaika na mikataba inayolitia hasara Tanesco, wameanza kujiandaa kuwekeza kwenye sekta hiyo.

Alisema kuwa, kimsingi ni muhimu kwa serikali kuhakikisha kuwa Tanesco inakuwa imara katika kipindi hiki cha ushindani, ambacho kinahitaji nguvu zaidi kwa shirika hilo la umeme ili kukabiliana na ushindani utakaotokana na kupitishwa kwa sheria hiyo.

Aliangaliza kuwa serikali inatakiwa kutambua kuwa Mtanzania wa leo anaitambua nchi yake na hivyo kuna umuhimu mkubwa kuwa na ufahamu kwamba mageuzi ya kiuchumi ni muhimu na sharti yajengwe palipo na mfumo imara wa usambazaji wa umeme.

Kwa upande wake Mbunge wa Moshi Mjini (Chadaema), Philemon Ndesamburo ambaye mbali
ya kuunga mkono hoja hiyo alishauri kuwa umeme usiwe kitu cha anasa na badala yake kiweze kupatikana kwa kila mtu anayekihitaji.

Mbunge huyo wa Moshi Mjini alishauri kuwa pamoja na umuhimu wa serikali kuingia katika mfumo huo mpya, jambo muhimu ni kuhakikisha kuwa maeneo ya mipakani yakatumia fursa ya kuwepo umeme kutoka nchi jirani.
Na Muhibu Said, Dodoma

Katibu Chadema, viongozi wa dini, wengine 12 watupwa rumande Buzwagi

KATIBU wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Wilaya ya Kahama , Lucas Petro (52) na wakazi wengine 13 , wamefikishwa mahakamani kujibu mashtaka ya kufanya mkusanyiko usio halali katika mgodi wa Buzwagi kushinikiza walipwe fidia.

Mratibu Msaidizi wa Polisi Mayila Kisanjo, aliwataja wengine Mahakama ya Wilaya ya Kahama mbele ya Hakimu Hassani kuwa ni Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Nyahanga, Simon Charles (45) , Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Chapulwa kupitia Chama cha Tanzania Labour (TLP), Tabo Majabi (48) na Juma Protas (40).

Mchungaji wa Kanisa la Assemblies of God (EAGT), Issa Issa (28), Mwalimu wa dini ya kiislamu Kahama Mjini, Jumanne Ntalula (48), balozi katika Kijiji cha Mwime na Mapande Machibya (56), ambaye ni mkulima kijiji cha Chapulwa.

Masanja Kashinje (50), Mathias John (45), Magaka Paulo (23), Bundala Makoye (26), Gema Maganga (41), wakazi wa Kijiji cha Mwendakulima.

Wengine ni Amos Malimi (53), mkazi wa Kijiji cha Mwime na Daudi Msuya (61), mfanyabiashara wa Kahama mjini.

Alidai kuwa washtakiwa hao wanadaiwa kufanya mkusanyiko usio halali katika lango la makao makuu ya mgodi huo, uliopo Kijiji cha Mwime kushinikizwa kulipwa fidia

Washtakiwa hao ambao walitiwa nguvuni juzi asubuhi, walikanusha mashtakana kupelekwa rumande katika Gereza la Wilaya ya Kahama hadi Mei 2, kesi yao itakapotajwa tena.

Na Zulfa Mfinanga, Shinyanga

Wakazi wa Buzwagi watawanywa kwa risasi, mabomu

Familia 500 zataka kurejea katika makazi yao mgodini

WANANCHI waliohamishwa kupisha ujenzi wa Mgodi wa Buzwagi, wilayani Kahama jana walitawanywa kwa risasi na mabomu ya kutoa machozi yaliyokuwa yakipigwa na Polisi kuzima jaribio lao la kutaka kurudi kwa nguvu katika makazi yao.


Jaribio hilo ambalo lilitangazwa juzi na wananchi hao lilianza alfajiri jana
baada ya wananchi hao kukusanyika kwa wingi wakiwa na mabango mbalimbali wakitaka kurudi kwa nguvu kwenye makazi yao ambayo yapo ndani ya uzio wa Mgodi wa Buzwagi.

Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Magesa Mulongo alisema kuwa kabla ya wananchi hao kutaka kuvamia kurudi kwenye makazi yao walisambaza ujumbe kwenye simu za mikononi ikiwemo simu yake unaodai kuwa umetoka kwa mtu mwenye nguvu ya kushawishi wananchi.

Mulongo alisema katika ujumbe huo, wananchi walidai kwa kuwa hawana uwezo wa kuinunua dola(serikali) ili iwatusaidie, watadai haki yao kwa kuweka rehani damu yao na kwamba ujumbe huo ulisambazwa kwa viongozi mbalimbali wa Serikali.

Alisema wananchi hao tayari wamelipwa fidia kwa asilimia 98, lakini baada ya kutumia vibaya fedha hizo, wamerudi kudai upya kwa maelezo kwamba walipunjwa wakati wa kuingia mkataba wa fidia na Kampuni ya Barrick.

Kufuatia tukio la jana, ambapo watu14 wanashikiliwa na polisi wilayani hapa, Mulongo alifahamisha kuwa wananchi hao walivamia mgodi huo kwa lengo la kuuhujumu.

Alisema licha ya Kamati ya Ulinzi na Usalama kuwazuia kuvamia eneo hilo, waligoma kuondoka kwa madai ya kwamba mpaka Mbunge wao James Lembeli afike mgodini hapo.

Wananchi hao waliokuwa wakipiga makelele wakidai kuwa wamiliki wa mgodi huo
ni makaburu na mafisadi, walidai kuwa mbuge wao aliwaagiza kuwa warudi katika
maeneo yao ambayo tayari walikwishalipwa fedha na nyumba zao kubomolewa kupisha ujenzi wa mgodi huo.

Kwa mujibu wa Mkuu wa Wilaya, kampuni ya Barrick ilikwishajenga nyumba 205 za fidia kwa wananchi walioondolewa, lakini nyumba 50 kati ya hizo bado zipo wazi baada ya wenyewe kugoma kuhamia, kwa sababu zisizoeleweka.

Mgodi huo wa Buzwagi umejumuisha vijiji vitatu, ambapo katika kijiji cha Mwendakulima tayari wote wameondoka na Mwime, familia tisa zimegoma huku zikiwa zimelipwa fidia na bado zimo ndani ya uzio wa kampuni hiyo.

Mulongo alisema kuwa katika Kijiji cha Chapulwa familia nne zimegoma kuondoka zikiwa zimelipwa fidia isipokuwa moja ambayo ilikataa kupokea.

Katika tukio la jana wananchi hao wapatao zaidi ya 500 walikuwa wamezingira lango
kuu la kuingia mgodini hapo.

Licha Mkuu Wilaya kuwata waondoke wakafanye mkutano katika ofisi za Serikali za Vijiji vyao ili kupata mwafaka wa haki zao, wananchi hao waligoma.

Baada ya kuona vurugu zinakuwa kubwa polisi waliingilia katina walianza kurusha risasi na mabomu ya kutoa hewani ili kuwatawanya wananchi.

Katika vurugu hizo watu 14 walikamatwa, lakini vinara wa vurugu hizo walitimua mbio kukwepa mkono wa sheria na polisi wanaendelea kuwasaka.

Kuanzia jana mgodi huo upo chini ya ulinzi mkali wa Jeshi la Polisi kutoka Shinyanga wakishiriana na wa wilayani Kahama.


Na Shija Felician, Kahama